Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya Waziri Mkuu

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana Dawa za Kulevya

( DCEA )

Cannabis

k

BANGI NI NINI?

Bangi ni aina ya dawa ya kulevya inayotokana na mmea unaoitwa “Cannabis sativa” ambao hustawi na hutumika kwa wingi hapa nchini na duniani kote. Bangi huathiri ubongo na kubadili jinsi tunavyotafsiri uhalisia wa vitu. Majani na maua ya mmea huo hukaushwa na hutumiwa kama kilevi peke yake au kwa kuchanganywa na dawa zingine. Mara nyingi bangi imekuwa ni kati ya dawa ya awali kutumiwa, ambapo watumiaji wengi huanza matumizi wakiwa na umri mdogo hivyo kuwa katika hatari zaidi kiafya, kijamii na kiuchumi. Aidha, watumiaji wengi wa bangi huishia kutumia dawa nyingine hapo baadae kama heroin na cocaine. Hivyo, bangi hutumika kama njia ya kuingia katika matumizi ya dawa nyingine za kulevya. Majina mengine ya bangi yanayotumika mitaani ni kama msuba, dope, nyasi, majani, mche, kitu, blanti, mboga, sigara kubwa, ndumu, msokoto, ganja, nk.

Bangi iliyokaushwa, mbegu na misokoto

kMADHARA YA BANGI

  • Bangi huamsha magonjwa ya akili hususani, ‘depression’, ‘anxiety’ ‘psychosis’na ‘schizophrenia’
  • Moshi wa bangi huzalisha lami na kemikali mbalimbali ambazo zinaweza kusababisha kansa ya mapafu
  • Bangi huathiri mifumo ya fahamu na kumfanya mtumiaji awe kwenye hali ya njozi ambapo ataona na kusikia vitu tofauti na uhalisia. Hali hii inachangia kupunguza stamina ya mtumiaji na kusababisha ajali, uharibifu wa mali pamoja na kushusha ufanisi wa kazi.
  • Baadhi ya watumiaji hupata wasiwasi mkubwa mara wavutapo na kuwahisi vibaya watu wanaowazunguka kuwa wanataka kuwadhuru au kuhisi wanajua kuwa wamevuta bangi. Wasiwasi huweza kumfanya mtumiaji amshambulie mtu na kumdhuru bila hatia
  • Mara baada ya kutumia bangi mapigo ya moyo huongezeka na mishipa ya damu kupanuka na hata kusababisha kiharusi.
  • Uvutaji wa bangi huweza kusababisha kikohozi sugu, kukosa pumzi, vidonda vya koo na pumu
  • Mtumiaji wa bangi hukosa mwamko wa maendeleo akijihisi ni mwenye maendeleo makubwa wakati anaishi maisha duni kabisa.
  • Matumizi ya bangi huchochea mmomonyoko wa maadili kutokana na ongezeko la vitendo vya uhalifu ikiwemo wizi, utapeli na ukatili wa kijinsia katika jamii.
  • Bangi husababisha utegemezi, huvuruga mahusiano ya kifamilia pamoja na upotevu wa ajira kwa mtumiaji. Matokeo ya kuvurugika mahusiano ni pamoja na kuwepo kwa migogoro isiyoisha, kutelekeza wenza na watoto, kuvunjika kwa ndoa, kutokuwa na ajira, ongezeko la watoto wa mitaani na biashara ya ngono.

Bangi iliyosindikwa

f

Matumizi ya bangi huchochea matumizi ya dawa nyingine za kulevya kwa namna mbili; kwanza kwa kuchanganya bangi na dawa nyingine za kulevya au kwa kuhamia kwenye dawa zingine kama heroin na cocaine. Hali hii huongeza madhara kwa mtumiaji na hata wakati mwingine husababisha vifo.

Kilimo haramu cha bangi mara nyingi hufanyika kwenye vyanzo vya maji, misituni na milimani ambapo miti hukatwa au kuchomwa moto na kusababisha kutoweka kwa baadhi ya viumbe hai na uoto wa asili, kukauka kwa vyanzo vya maji, mmomonyoko wa udongo na hatimaye ukame. Uharibifu huu umejidhihirisha katika safu za milima ya Uluguru, Usambara, Udzungwa na maeneo ya Arumeru.

Kushamiri kwa kilimo haramu cha bangi, kunaweza kusababisha uhaba wa mazao ya chakula na hivyo kupelekea kupanda bei ya vyakula na hata janga la njaa.

Kutokana na athari za matumizi na kilimo haramu cha bangi, Taifa linaingia gharama kubwa katika kukabiliana na tatizo hili, ikiwemo utoaji wa elimu mashuleni na katika jamii, matibabu ya maradhi mbalimbali, uteketezaji mashamba na udhibiti wa biashara haramu ya bangi.

Bangi huchangia kuongezeka kwa umasikini kwa mtumiaji, jamii na taifa kwa ujumla na kupelekea kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.

Mafuta ya bangi

gSheria inasemaje kuhusu bangi?

Kwa mujibu wa Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, sura ya 95, kilimo na biashara ya bangi katika Taifa letu ni KOSA LA JINAI. Kwahiyo, kujihusisha kwa namna yoyote na bangi (kulima, kuuza, kuhifadhi, kutumia, kuichakata, nk) ni KOSA LA JINAI na adhabu yake inafikia hadi KIFUNGO CHA MAISHA JELA.

Utamsaidiaje mtumiaji wa bangi?

Mtumiaji anaweza kupunguza kiasi anachotumia taratibu na hatimaye kuacha.Aidha, asasi za kiraia huwasaidia watumiaji kuacha kwa kuwapa unasihi. Nyumba za upataji nafuu ‘sober house’ ambako hupitishwa kwenye hatua 12 za upataji nafuu. Kwa msaada zaidi tembelea tovuti www.dcea.go.tz

Ujumbe kwa jamii

  1. Wazazi, walezi na jamii kwa ujumla tuwalee watoto na vijana wetu katika maadili mema kwa kuwasikiliza, kuongea nao na kufuatilia maendeleo yao mara kwa mara.
  2. Vijana wanashauriwa kujifunza na kuzingatia stadi za maisha ikiwemo kujiepusha na kukabiliana na makundi hatarishi yanayoweza kuwaingiza kwenye matumizi ya bangi.
  3. Waathirika wa matumizi ya bangi wasinyanyapaliwe badala yake wasaidiwe na waelekezwe kwenye huduma stahiki
  4. Bangi HAIONGEZI ufanisi na tija kazini, kwenye kilimo au masomo. Angalia jibu la swali hili hapa chini:-
Je, ni kweli bangi huongeza uwezo wa kusoma na kuelewa zaidi?

Hapana!. Bangi hufanya mishipa ya damu na ubongo kusinyaa, kunakosababisha kupungua kwa uwezo wa kufikiri na kumbukumbu. Kwa wanafunzi na vijana matumizi ya bangi hupunguza uwezo wao wa kufikiri, kusoma na kukumbuka na hii hupelekea kupata matokeo yasiyoridhisha katika masomo yao.