Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya Waziri Mkuu

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana Dawa za Kulevya

( DCEA )

Kupiga Vita Matumizi na Kusafirisha Dawa za Kulevya.

Imewekwa: 14 June, 2018
Kupiga Vita Matumizi na Kusafirisha Dawa za Kulevya.

Juni 26 ya kila mwaka, dunia inaadhimisha siku ya kupiga vita matumizi na kusafirisha dawa za kulevya. Mwaka huu, maadhimisho hayo yalifanyika kitaifa mkoani Mbeya kwenye Uwanja wa Ruanda Nzovwe ambako Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal alikuwa mgeni rasmi.

Pamoja na mambo mengine kwenye eneo hilo, walikuwapo watu wawili ambao walitoa ushuhuda wa madhara ya dawa za kulevya kwa binadamu na jamii kwa ujumla na kusababisha watu waliokuwapo kukumbwa na baridi ya woga kama mbwa aliyeona chatu.

Mashuhuda haoambao walisafirisha, walitumia kwa njia mbalimbali dawa za kulevya na hatimaye kujinusuru ni Very Fidelis Kunambina Rehema Chalamila maarufu kwa jina la Ray C.

Hata hivyo aliyewaliza wengi na kuwafanya wafikirie mengi ni Ray C ambaye leo tunalazimika kukuleta kauli yake yote akianza hivi,

“Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwa hapa leo nikiwa mzima mwenye afya na moyo wa ujasiri. Natumia fursa hii pia kuwashukuru Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya kwa kunialika kutoa ushuhuda wangu. Nafurahi kwa mahudhurio haya ya viongozi na wananchi, Nawapenda wote.

Naitwa Rehema Chalamila, wengi wananifahamu kwa jina la Kisanii la “Ray C”. Mungu alinibariki na kuwa mtu mwenye mafanikio makubwa kwani nikiwa na umri wa miaka 17 nilifanikiwa kupata kazi ya utangazaji katika Radio East Africa, mwaka 1999,mwaka 2000 nilijiunga na Radio Clouds. Mafanikio yangu hayakuishia hapo, nikiwa Radio Clouds mwaka 2002 nilianza muziki na kupata mafanikio makubwa sana. Mafanikio ambayo yaliniwezesha kujenga nyumba nzuri na kubwa nikiwa na umri wa miaka 19, baadaye kununua magari na kufungua maduka makubwa jijini Dar es Salaam na hatimaye kuwa msaada mkubwa wa familia yetu.

Aidha, nilitembelea Marekani,Dubai,Sweden,Hongkong,Uganda, Kenya, AfrikaKusini, , Uingereza, China, Oman, Australia, China, Norway,Msumbiji, Afrika Kusini, India, na Nigeria kufanya muziki.

Ghafla ujana ulionipaisha na kunipeleka juu ukanigeuza kichwa chini miguu juu. Nuru na nyota yangu ikafifia,Nikawa sionekani kiasi chawatu wakafikia kusema nimekufa.

Uwezo wangu wa kufanya muziki ulitoweka, nilianza kuuza vitu vyangu kimoja baada ya kingine nikianza na vidogo vidogo, mwisho nikauza magari yangu, Nyumba nayo ikaenda, Maduka nayo nikayafilisi nikafunga, nikaanza kuwa mtu wa kujificha huku nikendelea kudhoofika.

Ilifika wakati nililazimika kutembea nimevaa “kininja”. Mungu wangu! Nilikuwa nimenasa kwenye mdomo wa mamba, dawa za kulevya zilikuwa zinanimaliza! Nilipokuja kushtuka nilikuwa tayari nimenasa, Maisha yangu yakawa si starehe tena bali mateso na aibu!

Nilipokuwa katika uteja nilikwenda mbali zaidi ya kuuza vitu vyangu vya thamani. Roho inaniuma sana ninapokumbuka nilipomshikia kisu mama yangu mzazi kumlazimisha anipe hela nikanunue dawa.Roho inaniuma sana ninapokumbuka nilipomnyonga mkono mama kumpokonya simu.. ninapokumbuka haya roho huwa inaniuma kuliko hata kupoteza vitu vyangu vya thamani nilivyopoteza.